Na ina umuhimu gani ?

Maana ya bayoanuai

Bayoanuai inajumuisha aina yote ya viumbe duniani. Hii ni pamoja na aina milioni 8 ya mimea na na ya wanyama wanaopatikana kwenye sayari, mifumo ya ekolojia inayotumika kama makazi yake, na utofauti wa kimaumbile.

Bayoanuai ni changamano na ina mfumo unategemeana na kuingiliana kama utando na kila mshirika ana umuhimu wake na hutoa mchango hata wakati mwingine bila kutambulika. Aina nyingi ya chakula tunachokula, hewa tunayopumua, maji tunayokunywa na hali ya anga ambavyo hufanya sayari yetu kuwa mahali pazuri pa kuishi hutoka kwa mazingira.

Umuhimu wa bayoanuai

Bayoanuai ni nguzo inayofanya sayari yetu kuwa mahali pazuri pa kuishi. Bayoanuai huathiri vipengele vyote vya maisha ya binadamu, hutupa hewa safi na maji safi, hutupa lishe bora, hutupa uelewa wa kisayansi na madawa, huwezesha miili yetu kukabiliana na magonjwa na hukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Kwa kubadilisha au kuondoa kipengele chochote kwenye utando huo huathiri mfumo mzima wa maisha na kunaweza kusababisha madhara mabaya. Bila mazingira, hatuwezi kuishi duniani.

Athari ya shughuli za binadamu

Shughuli za binadamu zimesababisha mabadiliko kwa robo tatu ya ardhi na kwa theluthi tatu za maeneo ya bahari. Kati ya mwaka wa 2010 na 2015 tu, hekta milioni 32 ya misitu imetoweka; na kwa kipindi cha miaka 150 iliyopita, maeneo ya matumbawe hai yamepungua kwa nusu. Barafu inaendelea kuyeyuka kwa kiwango kinachotisha huku kukiwa na ongezeko la asidi kwenye bahari na kuihatarisha. Aina mbalimbali ya wanyamapori wanaendelea kuangamia zaidi ya mara kumi au mia zaidi ikilinganishwa na miaka milioni 10 iliyopita; na kwa kipindi cha miaka kumi ijayo, moja kati ya kila aina nne ya viumbe vinavyotambulika vinaweza kuangamia kabisa.

Idadi kubwa ya viumbe wako hatarini kuangamia; na tusipochukua hatua, uharibifu wa bayoanuai utasabababisha madhara kubwa mno kwa binadamu ikiwa ni pamoja na kuangamiza mifumo ya chakula na ya afya.

Uharibifu wa bayoanuai na COVID-19

Kuzuka kwa virusi vya COVID-19 ni ishara tosha kuwa tukiharibu mifumo ya ekolojia, tunaharibu mifumo inayowezesha binadamu kuishi. Tukiathiri uwezo dhaifu wa mazingira–kwa kukalia maeneo ya wanyamapori, kupunguza idadi ya ubayoanuai wa kimaumbile wa aina ya wanyama, kusababisha mabadiliko ya tabianchi na matukio mabaya mno yanayoathiri hali ya hewa–huwa tunasababisha ueneaji wa virusi kwa njia rahisi kutoka kwa wanyama hadi kwa wanadamu. Mazingira yanatupa ujumbe.

Ni wakati wa Mazingira

Kukabiliana na uharibifu wa bayoanuai ni njia ya pekee ya kuboresha sayari. Hili litawezekana tu iwapo tutaelewa kuwa viumbe wanategemeana na hufanya kazi kama mfumo mmoja. Ni wakati wa kutafakari kuhusu mahusiano yetu na mazingira na kuyafanya nguzo ya maamuzi yetu.

Mkataba wa Bayoanuai ya Kibayolojia unaainisha kuwa uanwai wa viumbe ni muhimu ili kuwa na sayari bora. Kwa kuzingatia haya, UNEP na wabia wenza wanasaidia nchi kuunda Mikakati ya Kitaifa ya Utekelezaji wa Mipango ya Bayoanuai. UNEP inasaidia majukwaa yanayotoa taarifa kuhusu mifumo ya ekolojia na bayoanwai kama vile Global Forest Watch, Global Peatlands Initiative na Interfaith Rainforest Initiative. Jifahamishe zaidi kuhusu bayoanuai hapa.